KIPA WA SIMBA KUPELEKWA INDIA KWA MATIBABU ZAIDI | BONGOJAMII

KIPA WA SIMBA KUPELEKWA INDIA KWA MATIBABU ZAIDI

Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya Bongojamii Blog kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka
BONYEZA HAPA KU-DOWNLOAD
KIPA wa Simba, Said Mohammed Nduda anatarajiwa kupelekwa India kwa matibabu ya goti lake la mguu wa kushoto.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa klabu ya Simba, Hajji Sunday Manara amesema leo kwamba Ndunda aliumia katika kambi ya Zanzibar kujiandaa na mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya mahasimu, Yanga SC Jumatano iliyopita.

Simba ilishinda kwa penalti 5-4 baada ya sare ya bila kufungana ndani ya dakika 90 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam langoni akiwa kipa namba moja, Aishi Salum Manula.

Manara amesema baada ya jitihada za awali za kumpatia matibabu kipa huyo bora wa michuano ya COSAFA mwaka huu, imeonekana anahitaji wataalamu waliobobea kumponya goti lake na sasa atapelekwa India.

Aidh, Hajji mtoto wa kiungo mshambuliaji wa zamani wa Yanga SC, Sunday Manara ‘Kompyuta’ amesema kwamba majeruhi mwingine wa muda mrefu, beki wa kulia, Shomari Salum Kapombe anaendelea vizuri na anatarajiwa kurejea uwanjani hivi karibuni.

Kuhusu majeruhi wengine, kiungo Haruna Niyonzima aliyeumia kwenye mchezo uliopita wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Ruvu Shooting, Simba ikishinda 7-0 na mshambuliaji John Raphael Bocco aliyeumia kwenye kambi ya Zanzibar pia nao wanatarajiwa kuanza mazoezi karibuni.

Baada ya usajili mzuri wa wachezaji nyota na waliobobea, Simba imekuwa na mwanzo mzuri msimu huu, kwani mbali na kubeba Ngao ya Jamii kwa ushindi wa matuta, pia imeanza vyema Ligi Kuu kwa ushindi mnono wa 7-0 dhidi ya timu ya Jeshi la Kujenga Taifa.

Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya Bongojamii Blog kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka

Featured Posts