Mahakama Yamkingia Kifua Mboe==>>Yaamuru Asikamatwe | BONGOJAMII

Mahakama Yamkingia Kifua Mboe==>>Yaamuru Asikamatwe

Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya Bongojamii Blog kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka
BONYEZA HAPA KU-DOWNLOAD
Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam imetoa zuio la muda kuzuia Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe asikamatwe na Polisi hadi maombi yake, aliyoyaomba ya kutaka asikamatwe, yatakaposikilizwa kesho.


Katika kesi hiyo ya kikatiba namba 1 ya mwaka 2017, Mbowe anapinga mamlaka ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum, Simon Sirro na Mkuu wa Upelelezi wa kanda hiyo (ZCO), Camilius Wambura, ya kutaka kumkamata hadi maombi hayo yatakaposikilizwa.


Maombi ya kesi hiyo yataanza kusikilizwa Februari 23, mwaka huu saa 7:30 mchana katika chumba cha wazi cha mahakama ili kuruhusu watu mbalimbali kusikiliza kesi hiyo.


Jopo la majaji watatu likiongozwa na Sekieti Kihiyo akisaidiana na Jaji Lugano Mwandambo na Jaji Pellagia Kaday lilitoa zuio hilo, hata hivyo walisema Polisi wanaweza kumuita Mbowe kwa mahojiano pindi watakapomhitaji.


Kesi hiyo ambayo ilisikilizwa kwa vipindi vitatu kuanzia saa 4 asubuhi hadi saa 7 mchana, mahakama iliamuru upande wa wadai ambao uliongozwa na Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu, kurekebisha maombi yao kwa kuwa hawakumuingiza Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) licha ya kuishitaki serikali.


Hali hiyo ilitokana na mawakili wa upande wa wadai, Lissu ambaye alipinga kitendo cha Mwanasheria wa Serikali, Gabriel Malata kuwatetea wadaiwa hao ambao ni RC, RPC na ZCO katika kesi hiyo kwa kuwa hawajaitaja serikali.


Akijibu hoja hiyo, Malata alidai kuwa waliofunguliwa madai hayo sio Makonda, Sirro wala Wambura, bali ni serikali hivyo ana mamlaka yote ya kuwawakilisha.


Baada ya pande zote kuwasilisha hoja zake, mahakama ilimruhusu Malata kuendelea kusikiliza kesi hiyo ambapo pia iliagiza upande wa wadai kufanya marekebisho ya maombi hayo na kumuongeza AG kama mdaiwa.


Hata hivyo, Lissu aliomba waruhusiwe kufanya marekebisho hayo kwa kumuongeza AG, ombi ambalo halikuwa na pingamizi.


‘’Tutafanya marekebisho ya maombi yetu na marekebisho mengine madogo madogo kwa namna tutakavyoona inafaa siku ya Jumatatu na tutawapa wajibu maombi Machi 6 mwaka huu na Machi 8 mwaka huu itatajwa kwa ajili ya kusikiliza maombi hayo,’’ alidai Lissu.


Mbowe aliwasili mahakamani hapo akiwa na gari lenye usajili namba T 830 aina ya Land Cruiser, saa chache kabla ya kesi yake kuitwa katika chumba namba 64 kwa ajili ya kusikilizwa.


Mbowe ambaye pia ni Mbunge wa Hai mkoani Kilimanjaro, alifika mahakamani hapo baada ya kutoka Kituo Kikuu cha Polisi saa 7 usiku, alikokuwa anahojiwa na kupekuliwa kuhusu sakata la dawa za kulevya.


Aidha, viongozi mbalimbali wa chama hicho wakiwemo Mbunge wa Kibamba, John Mnyika, Mbunge wa Bunda Mjini, Ester Bulaya, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa, madiwani na wafuasi wao walijitokeza kwa wingi, kusikiliza kesi hiyo huku wakifurahia amri ya mahakama ya kuzuia kutokamatwa kwa mwenyekiti huyo.


Katika kesi ya msingi, Mbowe anaomba mahakama iwazuie wadaiwa kutekeleza azma yake ya kumtia mbaroni, pia itoe amri ya kuwazuia kumkamata hadi hapo kesi hiyo ya kikatiba, itakapomalizika na kwamba polisi wasiendelee na mchakato wowote dhidi yake hadi hapo kesi hiyo itakapomalizika.


Anadai kuwa sheria inayompa Mkuu wa Mkoa mamlaka ya kutoa amri ya kumkamata na kumweka ndani mtu, iko kinyume cha katiba, kwa madai kuwa ilitungwa katika mazingira ambayo hapakuwa na vituo vya polisi vya kutosha.


Pia anadai kuwa kwa mazingira ya sasa, sheria hiyo imeshapitwa na wakati na anaiomba mahakama itamke kuwa ni kinyume cha katiba.


Mbowe pia anadai kuwa hata kama Mkuu wa Mkoa alikuwa anatekeleza mamlaka yake kwa mujibu wa sheria hiyo, basi hakutimiza matakwa ya kisheria, ambayo ni pamoja na kutoa taarifa kwa Hakimu wa Mahakama ya Wilaya au ya Hakimu Mkazi.


Vile vile, anaiomba mahakama kama itaona kuwa Mkuu wa Mkoa alikuwa sawa kutoa amri hiyo, basi imwamuru afuate matakwa ya kisheria, ikiwa ni pamoja na kulinda haki za binadamu katika kutekeleza madaraka yake hayo.

Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya Bongojamii Blog kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka

Featured Posts