MBUNGE NA MEYA WAZUIWA KUINGIA IKULU KWENYE KIKAO CHA RAIS | BONGOJAMII

MBUNGE NA MEYA WAZUIWA KUINGIA IKULU KWENYE KIKAO CHA RAIS

Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya Bongojamii Blog kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka
BONYEZA HAPA KU-DOWNLOAD
Mbunge wa Moshi Mjini, Japhary Michael, ameeleza kusikitishwa kwake juu ya maofisa usalama kuwazuia yeye na Meya wa Manispaa hiyo kuingia Ikulu ndogo ya Moshi kuhudhuria kikao cha Rais John Magufuli na viongozi wa dini.


Michael ambaye ni wa Chadema, alisema tukio hilo lilitokea juzi baada ya kufika Ikulu kutokana na mwaliko wa Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi kushiriki kikao hicho.


Mbunge huyo alisema aliitika mwaliko huo lakini ghafla akiwa kwenye foleni yeye na Meya wakazuiwa kuingia na kutakiwa warudi walikotoka.


Alisema alifika eneo la tukio saa 6.30 mchana akamkuta Mstahiki Meya akiwa ametangulia kwenye foleni.


“Tulipata mwaliko na tukaheshimu, ila katika mazingira ambayo hayaeleweki tulizuiwa na watu wa usalama na sisi hatukuhitaji kugoma tukaondoka,” alisema.


Alisema jambo la kusikitisha wakati akiwa kwenye foleni na viongozi wa dini, viongozi wa CCM na watendaji wengine wa Serikali, alichomolewa yeye na Mstahiki Meya wakiambiwa hawastahili kushiriki kika hicho.


Alisema Mkurugenzi alijaribu kuwatetea kwa kuwambia ndiye aliyewapa mwaliko kwa maelekezo ya Katibu Tawala wa Mkoa, hakusikilizwa kabisa.


“Mimi mbunge sijaumizwa, kwa kuwa nimetimuliwa bali ninasikitika kwa kuwa tunatiwa woga wa kushiriki shughuli za viongozi wetu wa kitaifa hasa wanapofanya ziara katika maeneo tunayowakilisha,” alisema.


Alisema kutokana na tukio hilo, huenda jamii ikawajengea taswira mbaya kwamba hawaheshimu viongozi wa kitaifa pale wasiposhiriki matukio mengine.


“Mimi binafsi nimetafsiri tukio hilo lililonipata kama ubaguzi wa kiitikadi kwa mambo ambayo ni ya kitaifa,” alisema.

Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya Bongojamii Blog kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka

Featured Posts