MISS TANZANIA 1996 SHOSE SINARE AWAJIA JUU WAPELELEZI | BONGOJAMII

MISS TANZANIA 1996 SHOSE SINARE AWAJIA JUU WAPELELEZI

Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya Bongojamii Blog kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka
BONYEZA HAPA KU-DOWNLOAD
Aliyekuwa Miss Tanzania mwaka 1996 Shose Sinare ameuomba upande wa mashitaka katika kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili, pamoja na wenzake wawili, walete mawasiliano yanayofanyika kati ya Tanzania na Uingereza juu ya upelelezi dhidi ya kesi yao.


Shose amedai hivyo jana katika katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Mkazi Cyprian Mkeha.

Mbali na Sinare, washitakiwa wengine ni katika kesi hiyo ni Kamishna Mkuu Mstaafu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Harry Msamire Kitilya, na Sioi Solomon.


Sinare alidai kuwa mpaka sasa wamekaa gerezani kwa zaidi ya mwaka na nusu hivyo upande wa mashitaka uwasilishe mawasiliano hayo.


Mapema, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Mutalemwa Kishenyi aliieleza mahakama kuwa upelelezi bado haujakamilika kwani bado wanasubiri awamu ya pili ya upelelezi huo.


Kufuatia hayo, Hakimu Mkeha ameahirisha kesi hiyo hadi Agosti 25 mwaka huu ili upande wa mashitaka ueleze muendelezo wa kile kilichowasilishwa kortini. 


Katika kesi hiyo washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka ya kula njama, kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kutakatisha fedha.


Wanadaiwa kutenda makosa hayo kati ya Machi 2013 na Septemba 2015 wakati wa mchakato wa mkopo wa dola za Marekani milioni 550 kwa serikali ya Tanzania kutoka Benki ya Standard ya Uingereza.


Katika kesi hiyo, inadaiwa kuwa Agosti 2, 2012 Sinare kwenye Makao Makuu ya benki ya Stanbic iliyopo Kinondoni kwa nia ya kudanganya aliandaa nyaraka ya pendekezo akijaribu kuonyesha kuwa Benki ya Standard ya nchini Uingireza ikishirikiana na benki ya Stanbic ya Tanzania watatoa mkopo wa dola za kimarekani milioni 550 kwa serikali ya Tanzania kwa ada ya uwezeshaji ya asilimia 2.4 ya kiasi cha mkopo huo wakati akijua kuwa sio kweli.


Inadaiwa kuwa Agosti 2, 2012 ,Sinare alitoa nyaraka za uongo za mapendekezo ya kuonyesha kuwa Benki ya Standard ya nchini Uingireza ikishirikiana na benki ya Stabic ya Tanzania, watatoa mkopo wa dola za kimarekani milioni 550 na kuziwasilisha katika ofisi za Wizara ya fedha wakati akijua kuwa sio kweli.


Aliendelea kudaiwa kuwa Septemba 20, 2012 katika Makao Makuu ya Benki ya Stanbic nchini yaliyopo Kinondoni, alitenda kosa la kughushi barua.


Sinare anadaiwa kughushi barua ya mapendekezo ikionyesha kuwa Benki ya Standard ya nchini Uingireza ikishirikiana na benki ya Stabic ya Tanzania watatoa mkopo wa dola za kimarekani milioni 550 kwa Serikali ya Tanzania kama ada ya uwezeshaji wa asilimia 2.4 ya kiasi cha mkopo huo wakati akijua kuwa sio kweli.


Agosti 21,2012, Sinare anadaiwa kuwa kwa lengo la kulaghai aliwasilisha nyaraka hizo za uongo kuiwezesha Serikali ya Tanzania kupata mkopo huo wa kiasi hicho cha ada ya uwezeshaji, katika ofisi za Wizara ya Fedha.


Washtakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kughushi nyaraka za makubaliano kwamba Novemba 5 ,2012 katika benki ya Stanbic makao makuu Kinondoni Dar es Salaam, kwa nia ya kudanganya walighushi waraka wa makubaliano wa Novemba 5, 2012.


Inadaiwa kuwa waraka huo ulikusudia kuonesha kuwa Stanbic Tanzania imeingia makubaliano ya ushirikiano na kampuni ya Enterpirise Growth Market Advisors (Egma) Limited kuwezesha upatikanaji wa mkopo wa Dola za Marekani milioni 550 kwa ajili Serikali ya Tanzania .


Wanadaiwa kuwa Machi 2013 jijini Dar es Salaam walijipatia Dola za Marekani milioni sita, wakionyesha kuwa fedha hizo zilikuwa ni malipo ya ada ya uwezeshaji upatikanaji wa mkopo na zililipwa kupitia Kampuni ya Egma T Ltd. Washtakiwa hao wanadaiwa kutakatisha fedha kwa kuhamisha, kuchukua na kuweka kiasi cha Dola za Marekani milioni sita katika akaunti tofauti tofauti za benki.


Kati ya Machi 2013 na Septemba 2015, wanadaiwa kuwa waliweka pesa hizo katika akaunti mbalimbali zilizomilikiwa na kampuni ya Egma na kwamba walipaswa kufahamu kuwa pesa hizo ni mazao ya uhalifu wa kughushi.

Bonyeza HAPA kudownload applicationi ya Bongojamii Blog kwenye simu yako ili kupata habari zetu Haraka

Featured Posts